Wednesday, August 1, 2012

RAIS CWT AFICHUA NAMNA SERIKALI ILIVYOWAFYEKA MISHAHARA WALIMU NA SIO KUWAONGEZA

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi Kawawa jijini Dar es Salaam wakionekana barabarani baada ya walimu wao kugoma. 
Rais wa CWT, Gratian Mukoba (kushoto)
Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Gratian Mukoba, amesema kuwa madai ya Serikali kwamba wamewaongeza walimu mshahara kwa asilimia 14 ni ya kinadharia zaidi kwani ukweli ni kwamba wamewapunguzia mshara kwa asilimia 5.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo, Mukoba alisema kuwa kauli ya serikali iliyorejewa na Waizir Kawambwa jana ni kinyume na uhalisia wa maisha, akifafanua kuwa hivi sasa, serikali yenyewe inakiri kupitia takwimu zake za kiuchumi kuwa mfumuko wa bei sasa umefikia asilimia 19, hivyo kudai kwamba wamewaongezea mshahara kwa asilimia 14 ni nadharia tu kwani kimahesabu, hiyo ni sawa na punguzo la asilimia tano katika kiasi wanachopata sasa.

"Walimu huwa tunafundisha hesabau za hasi na chanya... kama wameongeza asilimia 14 bila kutushirikisha, halafu mfumuko wa bei wa sasa ukaendelea kuwa asilimia 19, maana yake kilichotokea ni sawa na kulipa Sh. 14 katika deni la Sh. 19... hapo litabaki deni la Sh. 5.... kwahiyo kiuhalisia ni kwamba mshahara wa walimu umepunguzwa kwa asilimia tano," alisema Mukoba.

CWT imetangaza mgomo wa walimu katika nchi nzima kuishinikiza serikali itekeleze madai yao ya kuongezewa mshahara kwa asilimia 100, posho kwa asilimia 50 na 55 (kwa walimu wa sayansi) na pia kuwalipa posho ya mazingira magumu ya asilimia 30 ya mshahara.

Serikali imepinga mgomo huo kortini na kesho shauri lao linatarajiwa kutolewa hukumu na hakimu Sophy Wambura wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi Kanda ya Dar es Salaam.

KAFULILA AIRARUA BAJETI YA DK. MWAKYEMBE


*AHOJI KWANINI TAIFA LINAKOSA NDEGE HUKU RWANDA IKIWA NAZO SABA? KWANINI BADO TUNATUMIA RELI ILIYOCHOKA NA MELI CHAKAVU KAMA MWONGOZO ILIYONUNULIWA KARNE YA 18?

Mhe. David Kafulila

Mhe. Dk. Harrison Mwakyembe

Hamad... dege la Shirika la Ndege Tanzania (ATC) likionekana sakafuni baada ya kupata ajali mkoani Kigoma. 

Polisi wakiilinda ndege ya ATC iliyopata ajali mkoani Kigoma April, 2012. Kwa ndege kama hii, kwanini Kafulila asihoji suala la kuboresha usafiri wa anga?

Baadhi ya wananchi mkoani Kigoma wakiteremka kutoka kwenye meli ya Mv Mwongozo iliyonunuliwa na wakoloni kabla ya uhuru mwaka 1961... Kafulila anaitilia shaka meli hii kwa kudai kwamba sasa imechakaa mno!



Mbunge wa Kasulu Kusini,  David Kafulila (NCCR-Mageuzi), ameijia juu serikali na kutaka iwekeze vya kutosha katika kuimarisha miundombinu ya reli, ndege na meli ili hatimaye maisha ya Watanzania yaboreshwe na pia kuonyesha sababu za msingi za kuwaondoa wakoloni.

Kafulila ameyasema hayo bungeni  jioni hii wakati akichangia mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Uchukuzi inayoongozwa na Dk. Harrison Mwakyembe.

Alisema kuwa inasikitisha kuona kuwa hata baada ya miaka zaidi ya hamsini ya uhuru, Tanzania bado inategemea mioundombinu ya karne ya 18 iliyoachwa na wakoloni na kurudisha nyuma kasi ya wananchi katika kujiletea maendeleo.

Akitoa mfano, Kafulila alisema kuwa Tanzania ambayo ni nchi kubwa na yenye utajiri mkubwa wa rasilimali na pia ikijivunia hali ya amani na utulivu tangu ilipopata uhuru, bado inapitwa na nchi ndogo kama Rwanda katika usafiri wa ndege, licha ya kwamba nchi hiyo ni ndogo na tena inayokabiliwa na misukosuko mingi ya kisiasa na vita vya wenyewe kwa wenyewe.

 "Leo hii Rwanda ina ndege saba zinazofanya safari hadi hapa kwetu, sisi Tanzania hatuna ndege... kwanini?"

Kafulila alieleza kuwa inasikitisha kuona kwamba hadi sasa, wananchi wa Kigoma wanaendelea kutegemea usafiri wa meli ya Mv.Mwongozo kwenye Ziwa Tanganyika, ambayo ilinunuliwa na wakoloni kabla ya uhuru na sasa imechakaa mno, akitoa mfano kwa kusema kuwa: " mtu akipanda leo saa 8:00, anafika kesho... ni kwa sababu imezeeka."

Alisema kuwa Baba wa Taifa, Mwl. Nyerere alipigania uhuru kwa sababu wakoloni walikuwa wanachelewesha maendeleo, lakini mpaka sasa taifa linaendelea kutumia miundombinu ileile iliyojengwa na kununuliwa na wakoloni toka karne ya 18 wakati hivi sasa ni karne ya 21.



"Sasa kama bado tumebaki na vitu vilevile katika karne hii ya 21, kwanini basi tuliwaondoa wakoloni?" Alihoji na kushangiliwa na wabunge wengi, hasa wenzake wa upinzani.


Kati ya mambo ambayo Dk. Mwakyembe ameahidi kuyatekeleza katika bajeti ya wizara yake kwa mwaka ujao wa fedha ni pamoja na kununua ndege mbili za Shirika la Ndege Tanzania. 

RAIS KIKWETE ASISITIZA: SERIKALI HAIHUSIKI KIPIGO CHA DK. ULIMBOKA

Rais Jakaya Kikwete

Dk. Ulimboka akiwa hospitalini
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Kikwete, amesisitiza jioni hii kwamba serikali haikuhusika na wala haina sababu yoyote ya kumdhuru kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka.

Rais Kikwete ameyasema hayo jioni hii jijini Dar es Salaam wakati akiendelea kuzungumza na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari nchini.

"Hizi ni stori tu... nitamshangaa huyo mtu wa serikali kwenda kumpiga Dk. Ulimboka, kwa sababu ipi?" amesema.

Kikwete alitoa ufafanuzi huo kufuatia swali aliloulizwa juu ya uvumi ulioenea kuwa serikali,  kupitia Idara ya Usalama wa Taifa, ndiyo iliyohusika katika kumteka Dk. Ulimboka na kumtesa kabla ya kumtupa kwenye msitu wa Mabwepande jijini Dar es Salaam.

Dk. Ulimboka alikuwa mstari wa mbele wakati wa mgomo wa madaktari nchini na hivi sasa anaendelea kutibiwa nchini Afrika Kusini.



Hadi sasa, Rais Kikwete anaendelea kujibu maswali ya wahariri.

EPIQ BONGO STAR SEARCH KUBEBA WASHINDI 17 DAR

Mmoja wa vijana waliojitokeza kushiriki katika shindano la kusaka vipaji vya kuimba la Epiq Bongo Star Search akionyesha uwezo wake wa kupiga gita lililotengenezwa kienyeji nje ya ukumbi kabla ya kukutana na majaji kwenye fukwe ya Coco jijini Dar es Salaam leo. 
Sehemu ya vijana waliojitokeza kushiriki katika shindano la kusaka vipaji vya kuimba la Epiq Bongo Star Search wakiwa nje ya ukumbi kabla ya kukutana na majaji kwenye fukwe ya Coco jijini Dar es Salaam leo.
Majaji wa shindano la kusaka vipaji vya kuimba la Epiq Bongo Star Search (kutoka kushoto) Salama Jabir, Ritha Paulsen na Master Jay, wakiwa "mzigoni" kwenye fukwe ya Coco jijini Dar es Salaam leo. 
Mshiriki wa BSS akijaribu bahati yake mbele ya majaji

ZAIDI ya vijana 5,000 wamejitokeza katika usaili wa shindano la kusaka vipaji vya kuimba la Epiq Bongo Star Search katika fukwe za Coco leo.

Usaili huo ambao utakuwa ni wa siku tatu umeonekana kuwa ni wa aina yake hasa kutokana na idadi kubwa ya vijana waliojitokeza jana ikiwa ndio siku ya kwanza.


Katika sehemu mbalimbali za uwanja huo ilionekana kujazwa na vijana hao ambao wengi wao walikuwa wakiimba huku wengine wakiwa wanafanya mazoezi ya kutumia aina mbalimbali za vifaa vya muziki.


Akizungumzia shindano hilo, jaji mkuu wa Epiq BSS, Ritha Paulsen alisema kuwa Dar es Salaam ambao ndio mkoa wa mwisho katika usaili huo hamasa imekuwa kubwa sana kwa washiriki huku wengi wao wakiwa na matumaini makubwa ya kuchaguliwa.


"Tumeona vijana wazuri sana, na kama kawaida ya Dar tunatarajia ushindani mkali kwa mkoa huu, na ndio maana tutachukua vijana kumi na saba kutoka hapa," alisema Ritha.


Afisa Biashara wa Zantel, Sajid Khan, amepongeza umati mkubwa wa watu uliojitokeza kwa upande wa Dar es Salaam akisema kwa vipaji vilivyopatikana mwaka huu watu watarajie burudani ya kutosha vipindi vikianza kuonyeshwa kwenye luninga.


"Tunatoa zawadi kubwa kwa mwaka huu, Sh. milioni 50 pamoja na mkataba wa kurekodi, hivyo vijana wana kila sababu ya kujitokeza kwa wingi kutimiza ndoto zao," alisema Khan.


Zoezi hili litaendelea siku ya kesho (Alhamisi) na kesho (Ijumaa) ambapo washiriki 17 watakaopatikana wataungana na wengine 33 kutoka mikoani kufikisha idadi ya washiriki hamsini watakaoingia kambini.

LISSU NA OLE SENDEKA BWANA...! NDANI YA BUNGE WANAWESHEANA MOTO KINOMA, NJE NI SHWAAARI!


'Acha kuleta zako hizoo...!' Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (kushoto) akizungumza nje ya Bunge na Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka (kulia) huku wabunge wengine wakiwatazama na kucheka jana
Wabunge nchini wanaenzi sana amani. Licha ya tofauti zao za mara kwa mara bungeni na ambazo wakati mwingine huongozwa zaidi na ushabiki wa vyama vyao kiasi cha kuzomeana na hata kushtakiana mbele ya Spika wa Bunge. bado waheshimiwa hao huonekana kuwa ni kama marafiki wawapo nje ya 'mjengo' wa Bunge.

Hali hiyo ilijidhihirisha jana wakati Mhe. Tundu Lissu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki (CHADEMA) alipoonekana nje ya 'mjengo' akichati bila hofu na Mbunge wa Jimbo la Simanjiro (CCM), Mhe. Christopher Ole Sendeka.

Ikumbukwe kuwa juzi, Mhe. Tundu Lissu alimlipua Ole Sendeka wakati akizungumza na waandishi wa habari, akimtaja kuwa naye ni miongoni mwa wabunge wanaotuhumiwa kwa kashfa ya kutanguliza maslahi yao binafsi na kutumiwa kuwatetea wafanyabiashara wa mafuta walionyimwa tenda ya kuiuzia TANESCO mafuta ya kuendeshea mitambo ya kufua umeme ya IPTL.

Kutokana na Lissu kumtaja Ole Sendeka juzi, Mbunge huyo wa Simanjiro alikuja juu na jana akaomba mwongozo wa Spika ili ajue kama ibara ya 100 inayotoa kinga kwa wabunge inaweza kumkwaza katika kutimiza dhamira yake ya kumburuza Tundu Lissu mahakamani kutokana na kile alichodai kuwa ni kumdhalilisha kwa kumzushia mbele ya waandishi wa habari kuwa anatumiwa kuwatetea wafanyabiashara wa mafuta.

Hata hivyo, wakati akitoa ufafanuzi juu ya mwongozo alioomba Ole Sendeka, Spika wa Bunge, Mhe. Anna Makinda, alisema kuwa anampeleka Tundu Lissu katika Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ili awe shahidi namba moja kuthibitisha tuhuma kwamba kuna wabunge wanaokula rushwa na kutumiwa na wafanyabiashara na pia wengine hutetea maslahi yao binafsi kwa kufanya biashara na TANESCO.

Spika alisema vilevile kuwa ibara ya 100 inamkinga Lissu dhidi ya kusudio la kuburuzwa mahakamani kwa vile alizungumza na waandishi wakati akiwa kwenye eneo la Bunge. Akawasihi wabunge kuwa na subira wakati kamati ya uongozi ikishughulikia tuhuma za kashfa ya rushwa dhidi ya baadhi ya wabunge, hasa wa kamati aliyoivunja ya Nishati na Madini.

Licha ya mgongano wao wa ndani ya Bunge, waheshimiwa Ole Sendeka na Tundu Lissu walionekana nje ya Bunge baadaye wakizungumza pamoja pasi na kuonyesha dalili zozote za uhasama baina yao. Yaani ilikuwa ni amani, hakuna shari.

Je, wabunge wa nchi nyingine kama Kenya wanaweza? Safi sana!




SNOOP DOGG AACHA RAP NA KUGEUKIA REGGAE, SASA ABADILI JINA NA KUJIITA “SNOOP LION”


Sasa naitwa Snoop Lion...msanii Snoop Dogg akijiweka kwa pozi la picha jijini New York juzi  baada ya kutangaza kubadili jina lake.
Baada ya kumkamata mpakani akiwa na misokoto ya bangi, maafisa uhamiaji wa Norway waliwahi kumpiga marufuku kwa miaka miwili kuingia tena nchini mwao msanii aliyekuwa akifahamika awali kwa jina la Snoop Dogg.

Hata hivyo, maafisa hao wa Norway hawawezi kumzuia rapa huyo kubadili jina lake na sasa kujiita Snoop Lion.

Msanii huyo alitangaza juzi kuwa anabadili jina lake la awali ikiwa ni sehemu ya mikakati aliyo nayo sasa ya kujitambulisha kwa mashabiki kama nyota wa muziki wa reggae.

"Si nia yangu kuwavunjia heshima marapa wengine, lakini kamwe hawawezi kushindana na mimi katika rap," alisema wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini New York juzi.

"Nimeshinda kila tuzo ambayo msanii nyota anaweza kuipata katika muziki wa rap, katika rap wananiita 'Mjomba Snoop' . Wakati unapofikia hadhi ya kuitwa mjomba, ni vizuri sasa kugeukia kitu kingine."

Kutokana na jina lake la sasa, baadhi ya watu, akiwamo Dk. Ruth,  wamekuwa wakitania kwamba kuna siku msanii huyo ataiga jina la mijusi mikubwa na ya kutisha ya kale aina ya dinosaur na kujiita “Snoop Tyrannosaurus Rex”.

SOMA TAARIFA YA MNYIKA KUHUSU RUFAA YAKE KATIKA TUHUMA ZA EPA DHIDI YA MWIGULU NCHEMBA NA JINSI ALIVYOMCHANA MWENYEKITI JENISTA MHAGAMA


RUFAA YANGU KATIKA TUHUMA ZA EPA NA MWIGULU NCHEMBA 

Mhe. John Mnyika
Mhe. Mwigulu Nchemba
Mhe. Jenista Mhagama
Na John Mnyika
Nimekata Rufaa dhidi ya uamuzi wa Mwenyekiti Mhagama suala la EPA; nasubiria Spika aitishe kamati ya kanuni ili bunge liendeshwe kwa ufanisi:
Katika kipindi cha takribani wiki mbili nimeulizwa kwa nyakati mbalimbali na wananchi kwenye mitandao ya kijamii na wanahabari kwa njia ya simu kutaka kufahamu iwapo nilitimiza azma ya kukata rufaa juu ya uamuzi wa Mwenyekiti wa Bunge Jenister Mhagama kutoa muongozo wa kunitaka kuwasilisha ushahidi katika suala alilolisema yeye mwenyewe badala ya kunipa fursa ya kueleza tuhuma nilizonazo dhidi ya Mwigulu Nchemba na hatimaye kuwasilisha ushahidi juu ya tuhuma hizo.
Kwa kuwa swali na suala hilo limekuwa likirudiwarudiwa kwenye mijadala mbalimbali bila taarifa sahihi kutolewa, naomba kutoa majibu kwamba tayari nilishawasilisha malalamiko kwa mujibu wa Kanuni ya 5(4) ya Kanuni za Kudumu za Bunge toka tarehe 12 Julai 2012 dhidi ya uamuzi huo wa Mwenyekiti wa Bunge ambao haukuzingatia matakwa ya Kanuni za kudumu na uendeshaji bora wa Bunge.
Ninachosubiria sasa ni Spika kuitisha kikao cha kamati ya kanuni kwa mujibu wa kanuni ya 5(5) ya kanuni za Kudumu za Bunge na kulijulisha bunge kuhusu uamuzi utakaotolewa.
Nimekata rufaa kwa sababu tatu:  mosi; mwenyekiti amenitaka kuwasilisha ushahidi wa suala ambalo sikulisema mimi bali amelisema yeye; pili, Sikupewa nafasi ya kueleza tuhuma nilizotaka kueleza dhidi ya Mheshimiwa Mwigulu Lameck Nchemba na badala yake Mwenyekiti aliendelea kunitaka nizungumzie tuhuma alizozieleza yeye; mwenyekiti hakufanya uamuzi kuhusu suala ambalo nililiombea kuhusu utaratibu kwa mujibu wa kanuni ya 64 (1) (a) juu ya madai ya Mwigulu Lameck Nchemba juu ya hotuba ya kambi rasmi ya upinzani ya Ofisi ya Rais.
Katika barua yangu kwa katibu wa Bunge nilieleza pia kuwa ni muhimu kamati ya kanuni ikakutana kabla ya kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kushughulikia uamuzi uliofanywa na Naibu Spika Job Ndugai tarehe 12 Julai 2012 katika kikao cha ishirini na mbili cha mkutano wa nane kwamba “Kamati hiyo sasa ndiyo itashughulikia ushahidi huo na kuthibitisha kwamba Mheshimiwa Mwigulu  naye kumbe alikuwa anahusika na wizi wa fedha za EPA”, ili kamati hiyo isifanye uamuzi kwa kurejea muongozo usiokuwa sahihi.
Ikumbukwe kwamba kwa mujibu wa  kumbukumbu rasmi ya Bunge (Hansard) za kikao cha kumi na tano cha tarehe 3 Julai 2012 cha mkutano wa nane wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mwenyekiti wa Bunge Jenister Mhagama alisema na kufanya maamuzi kwamba: “Mheshimiwa Mnyika, umesema kwamba unao ushahidi, naomba unisikilize kusudi utakaponijibu ujibu mwongozo nitakaokupa kwa mujibu wa taratibu. Mheshimiwa Mnyika umesema hapa na kulithibitishia Bunge, waheshimiwa wabunge naomba tusikilizane. Umesema unao ushahidi na umelithibitishia Bunge kwamba yeye Mheshimiwa Lameck Mwigulu Nchemba ni mmoja wa watuhumiwa katika kesi hizo za EPA. Sasa na mimi nakupa siku saba ulete ndani ya Bunge tuhuma zinazomgusa Mheshimiwa Mwigulu.”
Katika rufaa yangu nimeeleza kutoridhika dhidi ya  muongozo huo wa Mwenyekiti wa Bunge na kwa kutumia kanuni ya 5 (4) nimewasilisha sababu za kutoridhika na uamuzi huo kama ifuatavyo:
Sababu ya Kwanza; Mwenyekiti amenitaka kuwasilisha ushahidi wa suala ambalo sikulisema mimi bali amelisema yeye:
Kwa mujibu wa kumbukumbu rasmi za Bunge sikutamka maneno kwamba ninao ushahidi wa kulithibitishia bunge kwamba Lameck Mwigulu Nchemba ni mmoja wa watuhumiwa wa kesi hizo za EPA  kama ambavyo amedai Mwenyekiti wa Bunge kama nilivyomnukuu hapo juu.
Nilichokisema, na nanukuu: 
“Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nasimama kwa kanuni ya 64 (1) (a) hatatoa ndani ya Bunge taarifa ambazo hazina ukweli, Mheshimiwa Mwenyekiti, mzungumzaji anayezungumza ili aelewe kwamba anachokisema anakitambua; alikuwa mtumishi wa Benki Kuu ambayo ilikumbwa na kashfa ya ufisadi wa EPA na sasa ni Mweka Hazina wa Chama cha CCM inayotuhumiwa kwenye wizi wa pesa za KAGODA... lakini usalama wa taifa hatujawahi kusikia popote katika kuzuia. Usalama wa Taifa kuhusika kwenye kuzuia. Kwenye Bunge hili, kambi ya upinzani ilileta ushahidi wa Barua ya usalama wa Taifa kwenye kashfa hiyo ya EPA ambayo anaifahamu vizuri . Usalama wa taifa ukizuia jambo lisije bungeni kujadiliwa badala ya kuibua ufisadi, kuzuia ufisadi usitokee, ushahidi huo uko ndani ya kumbukumbu za Bunge na ukitaka nilete ushahidi wa namna gani matukio ya uhalifu na hili ni lalamiko ndani ya idara ya usalama wa taifa ya watumishi wa usalama wa taifa wanatoa ushirikiano ,wanatoa taarifa viongozi wa juu yao hawazishughulikii  taarifa  na katika hotuba ya ofisi ya rais haijatuonyesha popote idara ya usalama wa taifa ilipozuia matukio ya uhalifu kwenye hotuba hii tunayozungumza. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba mchangiaji atambue huo ukweli na aache propaganda na aache siasa kwa sababu yeye ni mmoja wa watuhumiwa”
Sababu ya Pili; Sikupewa nafasi ya kueleza tuhuma nilizotaka kueleza dhidi ya Mwigulu Lameck Nchemba na badala yake Mwenyekiti aliendelea kunitaka nizungumzie tuhuma alizozieleza yeye.
Kwa mujibu wa kumbukumbu rasmi za Bunge (Hansard) niliposema “aache propaganda  na aache siasa kwa sababu yeye ni mmoja wa watuhumiwa”, Mwenyekiti aliingilia kati kabla ya mimi kueleza kuwa yeye ni mmoja wa watuhumiwa wa nini na kuelekeza ifuatavyo:
 “Mheshimiwa Mnyika, naomba uthibitishe hilo kwamba na yeye ni mmoja wa watuhumiwa kabla sijatoa mwongozo na kama unao uthibitisho kwamba na yeye ni mmoja wa watuhumiwa naomba utoe uthibitisho huo kama huna ufute kauli yako ili niweze kufanya maamuzi ya kinachofuata ili tuendelee na kazi za kuwawakilisha wananchi. Mheshimiwa Mnyika una uthibitisho wa kwamba Mheshimiwa Mwigulu ni mmoja kati ya wanaotuhumiwa?
Nilipoanza tu kueleza kuwa:“Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuwa mmoja wa watumishi wa Benki Kuu...” kabla hata ya kuendelea kueleza ni mtuhumiwa wa nini katika taasisi ambazo nilitaka yeye alizitumikia au anaendelea kuzitumikia Mwenyekiti akanikatisha na kudai yafuatayo “Mheshimiwa Mnyika umesema hapa na kulithibitishia (bunge)”.
Ilibidi niingilie kati na kuomba tena haki ya kueleza ni Mwigulu Lameck Nchemba ni mmoja kati ya wanaotuhumiwa na nini kwa kumuomba Mwenyekiti anipe haki ya kujieleza na kueleza tuhuma kama ifuatavyo:
“Niambie kwanza niseme tuhuma gani ninazo dhidi yake na nitoe ushahidi wa hizo tuhuma. Nimesema ni mmoja wa watuhumiwa. Niruhusiwe niseme anazotuhuma gani na nitoe ushahidi wa hizo tuhuma.”
Hata hivyo Mwenyekiti alikataa kunipa nafasi ya kueleza tuhuma nilizotaka kueleza dhidi ya Mwigulu Lameck Nchemba na badala yake Mwenyekiti akafanya uamuzi wa kunitaka nilete ushahidi wa tuhuma alizozieleza yeye.
Sababu ya Tatu; Mwenyekiti hakufanya uamuzi kuhusu suala ambalo nililiombea kuhusu utaratibu kwa mujibu wa kanuni ya 64 (1) (a) juu ya madai ya Mwigulu Lameck Nchemba juu ya hotuba ya kambi rasmi ya upinzani ya Ofisi ya Rais:
Nilitaka utaratibu ili aweze kuondoa maneno potofu aliyoyatoa huu ya nukuu juu ya ukweli ambao kambi rasmi ya upinzani iliueleza kwamba “…. Usalama wa Taifa hatujawahi kusikia popote wamehusika katika kuzuia mchakato huo japokuwa wanakuwa na taarifa za kutosha.”
Hata hivyo, Mwenyekiti hakufanya uamuzi kuhusu suala hilo ambalo nilitangulia mimi kuliomba badala yake akaishia kunitaka kuleta ushahidi wa tuhuma alizozieleza yeye mwenyewe mwenyekiti bila kufanyia kazi utaratibu ambao niliomba uzingatiwe. Hali ambayo inaweza kutafsiriwa kuwa ulikuwa ni upendeleo kwa Mwenyekiti hakumkatisha Nchemba alipotoa tuhuma dhidi ya kambi rasmi ya upinzani kumtaka athibitishe alipotajwa tu ni mmoja wa watuhumiwa bila tuhuma hizo kuelezwa Mwenyekiti alitoa muongozo wa tuhuma alizozisikia yeye na kutaka ushahidi uletwe kwa tuhuma hizo.
Pamoja na kuwawakilisha wananchi katika masuala mengine ya maendeleo bungeni, hatua hii ya kukata rufaa inalenga kudumisha ukweli na kuhakikisha kwamba bunge linaendeshwa kwa kuzingatia kanuni bila upendeleo ili kuweza kutimiza wajibu wa kikatiba wa kuisimamia serikali kwa ufanisi zaidi.
Wako katika kuwawakilisha wananchi,

John Mnyika (Mb)

BAHANUZI, CHUJI, BOBAN, REDONDO WAITWA STARS

Said Bahanunzi

KOCHA Kim Poulsen leo amemuita kwa mara ya kwanza mfungaji bora wa michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Said Bahanuzi wa Yanga, katika kikosi chake cha wachezaji 21 wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, kitakachocheza mechi ya kirafiki ugenini Agosti 15 dhidi ya timu ambayo bado haijatajwa.

Pamoja na mshambuliaji huyo aliyejiunga na Yanga katika kipindi hiki cha usajili akitokea Mtibwa Sugar ya Manungu, Kim pia amemrejesha kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2010 kiungo Athuman Idd 'Chuji' aliyeng'aa katika michuano iliyomalizika Jumamosi ya Kombe la Kagame ambayo klabu ya Yanga ilitwaa ubingwa wa pili mfululizo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Kim pia amemrejesha kikosini kiungo 'fundi' wa Simba, Haruna Moshi 'Boban' ambaye aliachwa na kocha aliyepita, Jan Poulsen, kufuatia kukacha kwenda kuchezea timu ya vijana kwa nia ya kuangalia uwezo wake.

Kocha huyo Mdenmark pia amemjumuisha katika kikosi chake kiungo wa Azam, Ramadhani Chombo 'Redondo' wakati makipa ni Juma Kaseja (Simba), Mwadini Ali (Azam) na Deogratius Munishi 'Dida' wa Azam, ambaye aliisaidia timu yake kufika fainali ya Kombe la Kagame, ambapo ililala 2-0 dhidi ya Yanga. 


Hata hivyo, Kim amemfumbia macho beki wa kati Nadir Haroub 'Cannavaro', licha ya mlinzi huyo kutengeneza ukuta mgumu pamoja na Kelvin Yondani na kuisaidia timu yao ya Yanga kutwaa ubingwa wa pili mfululizo wa Kombe la Kagame. 

 Wachezaji walioitwa Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager wanatakiwa kuripoti kambi kwenye hoteli ya Tansoma, Dar es Salaam, Agosti 8 mwaka huu saa 1 jioni tayari kwa mazoezi yatakayoanza siku inayofuata.

Makipa walioitwa kwenye kikosi hicho ni Deogratias Munishi (Azam), nahodha Juma Kaseja (Simba) na Mwadini Ali (Azam). Mabeki ni nahodha msaidizi Aggrey Morris (Azam), Erasto Nyoni (Azam), Kelvin Yondani (Yanga) na Shomari Kapombe (Simba).

Viungo ni Athuman Idd (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Haruna Moshi (Simba), Mrisho Ngassa (Azam), Mwinyi Kazimoto (Simba), Ramadhan Chombo (Azam), Ramadhan Singano (Simba), Salum Abubakar (Azam) na Shabani Nditi (Mtibwa Sugar).

Wachezaji wanaounda safu ya ushambuliaji ni John Bocco (Azam), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), Said Bahanuzi (Yanga), Simon Msuva (Yanga) na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC).

MWANDOSYA: NILIMUOMBA MUNGU ANIPE JAPO DAKIKA 5 NIJE KUSHUKURU BUNGENI

Prof. Mark Mwandosya

Aisee angalia usije ukateleza...! Rais Jakaya Kikwete akitaniana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Prof. Mark Mwandosya

WAZIRI wa Nchi katika Ofisi ya Rais Asiye na Wizara Maalum, Profesa Mark Mwandosya, amerejea bungeni kwa mara ya kwanza leo katika kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja kutokana na matatizo ya kuugua yaliyomfanya atumie kipindi chote hicho katika matibabu, yakiwamo aliyoenda kuyapata nchini India.

Profesa Mwandosya aliutumia muda wake wa kuzungumza bungeni kuwashukuru wabunge, Watanzania na wote walioshiriki kumsaidia na kumuombea katika kipindi kigumu cha ugonjwa.

"Ukiugua kumbe kunakuwa hamna chama. Tofauti zote za kiitikadi zinawekwa pembeni watu wanaungana kwa ajili ya kukuombea bila ya kujali ni chama gani," alisema.

"Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuwa hapa leo. Nawashukuru wote kwa sapoti yenu. Namshukuru pia Rais Jakaya Kikwete, alinisisitiza kwamba afya kwanza. Aliniambia usifikirie kwamba sijui kuna kijiji fulani hakina maji. Shughulikia afya yako kwanza. Na kweli, ona sasa mimi si Waziri wa Maji tena.

"Kwa hakika nilikuwa katika kipindi kigumu. Nilimuomba Mungu anipe japo dakika tano nije nizungumze tena hapa (bungeni) na wenzangu.

"Napenda kuwasisitiza kwamba daima tupime afya zetu. Mimi nilikuwa sijakiona kitanda (kulazwa kwa ugonjwa) kwa miaka 45. Nilidhani mimi ni mzima sana kwa sababu nafanya mazoezi kila siku, lakini kumbe bado ni binadamu tu na Mungu ana mipango yake. Tupime afya kila mara," alisisitiza Mwandosya katika muda wake wa kuzungumza ambao aliutumia wote kutoa shukurani zake.

"Katika kipindi chote hicho, nimebaini kuwa kumbe kwenye kuumwa hakuna siasa... watu wengi walinijulia hali na kunitakia uzima bila kujali kuwa ni wa CCM, Chadema, TLP na vyama vingine," aliongeza Prof. Mwandosya.

Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni leo, ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Mbunge wa Kigoma Kaskazini,
Mhe. Zitto Kabwe, alisimama na kusema wao kama kambi ya upinzani wanamtakia afya njema Profesa Mwandosya na wanamkaribisha kwa mikono miwili.