Mhe.John Mnyika |
Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA) amepewa siku saba kuanzia
leo kuthibitisha tuhuma za wizi wa fedha za Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje
(EPA) dhidi ya Mbunge wa Iramba, Lameck Mwigulu Mchemba.
Mnyika alitakiwa kufanya hivyo na Mwenyekiti wa Bunge, Mhe. Jenista
Mhagama, baada ya kuibuka majibizano makali wakati Mwigulu akichangia hoja ya
makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Rais (Utawala Bora).
Awali, Mnyika aliomba mwongozo wa Spika na kupinga baadhi ya
maelezo ya Mwigulu ambaye katika mchango wake, aliponda baadhi ya taarifa zilizomo kwenye
hotuba ya Waziri Kivuli wa Kambi Rasmi ya Upinzani, ikiwemo iliyodai kuwa hali
ngumu ya watumishi wa serikali imewafanya walimu wa shule za msingi kujikuta
wakijihusisha na biashara huku wahadhiri wa vyuo mbalimbali vya umma wakilazimika
kufundisha pia katika vyuo vingine binafsi hadi vitatu.
Wakati mabishano hayo, yakiendelea na wakati fulani kuwahusisha wabunge
wengine kama Mchungaji Msigwa wa Jimbo la Iringa Mjini (CHADEMA) na Mhe. George
Simbachawene wa Kibakwe(CCM), ndipo Mnyika alipomtuhumu Mwigulu kuwa naye ni
miongoni mwa watuhumiwa wa kashfa ya fedha za EPA (Sh. bilioni 133) kwani
alikuwa ni miongoni mwa watumishi wa Benki Kuu ya Tanzania ambako ndiko wizi
huo ulipotokea.
Alisema kwamba inasikitisha kuona kuwa hotuba ya bajeti ya
Ofisi ya Rais (Utawala Bora) haionyeshi ni kwa jinsi gani Idara ya Usalama wa Taifa
imekuwa ikizuia uhalifu kama wa EPA.
Kauli ya kumtuhumu Mwigulu ndiyo iliyomfanya Mwenyekiti (Jenista
Mhagama) kumpa siku saba ili athibitishe tuhuma hizo.
Hata hivyo, Mwigulu
aliposimama tena, alianza kwa kusema kuwa wakati wizi wa EPA ukitokea (mwaka
2005), yeye alikuwa bado ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kwamba,
(wakati huo) hata mlango wa kuingilia
Benki Kuu alikuwa haujui. Alisema kuwa
alianza kazi BoT Oktoba, 2006.
No comments:
Post a Comment