Saturday, July 14, 2012

MAXI RODRIGUEZ AONDOKA LIVERPOOL


Maxi Rodriguez wa Liverpool akishangilia baada ya ushindi wao katika mechi ya fainali ya Kombe la Carling dhidi ya  Cardiff City kwenye Uwanja wa Wembley Februari 26, 2012 mjini London, England. Liverpool walishinda kwa penalti 3-2.
MAXI Rodriguez ameondoka Liverpool baada ya miaka miwili na nusu na kurejea katika klabu yake ya zamani ya Newell's Old Boys ya Argentina.

Kiungo Rodriguez, 31, aliwasili Anfield akitokea Atletico Madrid Januari 2010, na amefunga magoli 17 katika mechi 73 alizoichezea Liverpool.

"Narudi nyumbani na begi la kumbukumbu nzuri," alisema Rodriguez katika barua ya wazi kwa mashabiki iliyochapishwa kwenye tovuti rasmi ya Liverpool.

"Nashukuru kwa sapoti yenu."

Rodriguez alikuwa na mwaka mmoja umebaki katika mkataba wake, lakini Liverpool hawajabainisha kama kuna ada ya uhamisho imehusika katika kurejea kwake Amerika Kusini.

Lakini kuondoka kwake ni pigo kwa kocha mpya Brendan Rodgers, ambaye alidhamiria kumbakisha Muargentina huyo.

Rodriguez, ambaye alianza maisha yake ya soka katika klabu ya Newell's Old Boys, alichezeshwa mara chache sana Liverpool msimu uliopita, akifunga magoli sita katika mechi 21 za michuano yote.

"Kabla ya kujiunga na Liverpool, niliiona klabu hii kama moja ya taasisi kubwa katika soka," aliongeza Roriguez katika barua hiyo ya wazi.

"Baada ya muda wangu hapa naweza kuthibitisha kwamba hii sio tu klabu kubwa, bali pia ni familia bora."

Taarifa katika tovuti ya Liverpool ilisema:  "Kila mtu hapa Liverpool FC anapenda kumshukuru Maxi kwa mchango wake klabuni na kumtakia maisha mema huko aendako."

No comments:

Post a Comment