ASEMA MAHAKAMA ND’O ITAJUA KAMA KWELI MTUHUMIWA NI MGONJWA WA AKILI AMA LA |
Kamanda Kova (kushoto) akifafanua jambo. |
Dk. Ulimboka akiendelea na matibabu. |
Siku moja tu baada ya Mchungaji Gwejima wa Kanisa la Ufufuo na
Uzima lililopo Kawe jijini Dar es Salaam kupinga maelezo ya Polisi kuhusiana na
madai ya kuungama kwenye kanisa lake kwa Mkenya Joshua Mhindi (31) aliyedaiwa
kukiri kuwa alishiriki kumteka na kumtesa Dk. Steven Ulimboka; Kamanda wa
Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova ameibuka leo na kusema
kuwa kamwe hayuko tayari kmujibu Mchungaji huyo.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo,
Kova amesema kuwa hawezi kumjibu Gwejima kwa vile anatambua
kuwa suala hilo limeshatua mahakamani na kuendelea kulizungumzia ni sawa na kuingilia
uhuru wa mahakama, kitendo ambacho ni ukiukwaji wa sheria za nchi.
Kova ameyasema hayo wakati alipokutana na waandishi wa habari
kuzungumzia hali ya uhalifu jijini kwa kipindi cha kuanzia Januari hadi hadi
sasa.
“Najua mnaningoja kwa hamu niizungumzie taarifa iliyotolewa
na Mchungaji Josephat Gwejima wa Kanisa la Ufufuo kuhusiana na mtuhumiwa Mhindi…
nasema siwezi kuliongelea suala hilo kwa kuwa liko mahakamani na katiba ya nchi
inazuia kuzungumzia suala lililoko
kwenye mhimili huo nje ya mfumo wa mahakama. Labda niseme kwamba, ile taarifa
ya awali niliyowapatia Julai 13 inabaki kama ilivyo kwa kuwa ina maelezo na
ushahidi wote juu ya suala hili,” amesema Kamanda Kova.
UGONJWA WA AKILI WA MTUHUMIWA
Hata hivyo, licha ya Kamanda Kova kukataa kuzungumzia kwa
undani juu ya taarifa ya Mchungaji Gwejima, aligusia suala alilosema mchungaji
(Gwejima) kuwa huenda mtuhumiwa huyo ana matatizo ya akili; akisema kwamba sheria
za nchi zinawakumba watu wote wanaotenda makosa ya jinai, wakiwemo wenye
matatizo ya akili.
“Kama Mhindi ana matatizo ya akili atapelekwa kwa daktari kwa
ajili ya kujua ukweli wa hali aliyokuwa nayo wakati akitenda kosa hili, kama
alikuwa ana kichaa kamili, kichaa nusu au la, mahakama ndiyo inayojua namna ya kushughulika
na watu wenye kesi kama hizi,” alisema.
Aliwataka wananchi waendelee kwenda kuungama kwa viongozi wa
dini, lakini akaonya kwamba jeshi la polisi kamwe haliko tayari kumuacha mtu
aliyekiri mwenyewe kwamba ametenda jinai kwani sheria utachukua mkondo wake.
Jana, wakati wa mahubiri ya ibada ya Jumapili, Mchungaji Gwejima
alikana taarifa zilizotolewa na Kamanda Kova kuwa mtuhumiwa Mhindi ambaye ni
raia wa Kenya alienda kanisani kwao kuungama na kukiri kwamba alishiriki kumteka
na kumtesa Dk. Ulimboka kwa kushirikiana na wenzake wa kikundi cha Kenya cha Gun
Star.
Hivi sasa, Dk. Ulimboka ambaye ni kiongozi wa Jumuiya ya Madaktari anaendelea na matibabu nchini Afrika Kusini. Alikuwa mstari wa mbele wakati wa mgomo wa madaktari uliofanyika hivi karibuni na katikati ya mgogoro huo akakumbwa na kadhia ya kutekwa na watu wasiojulikana, akapigwa na kuteswa vibaya kabla ya kutupwa katika msitu wa Mabwepande jijini Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment