Saturday, June 30, 2012

IRINGA YAZINDUKA COPA COCA-COLA

IRINGA imezinduka kwenye michuano ya Copa Coca-Cola baada ya leo asubuhi (Juni 30 mwaka huu) kuifunga Kaskazini Pemba mabao 3-0 katika mchezo uliofanyika kwenye Uwanja wa Nyumbu mkoani Pwani.
 
Hadi dakika 45 za kwanza za mechi hiyo ya Kundi B zinamalizika matokeo yalikuwa suluhu. Mabao ya washindi yalifungwa na Goodluck Jonas dakika ya 51, Musa Maginga dakika ya 67 na Ramadhan Kiwelu dakika ya 70.
 
Iringa ilipoteza mechi zote mbili za kwanza dhidi ya Mwanza na Mjini Magharibi. Mbele ya Mwanza ilifungwa 3-1 wakati kwa Mjini Magharibi ikachezea kichapo cha mabao 3-0.
 
Katika mechi nyingine zilizochezwa asubuhi, Tabora iliichapa Shinyanga mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam. Mabao hayo yalifungwa na Said Juma na Ramadhan Mbalamwezi katika kila kipindi.
 
Nayo Ilala imepata pointi yake ya kwanza katika michuano hiyo baada ya kutoka suluhu na Kusini Pemba katika mechi ya kundi A iliyochezwa Uwanja wa Tanganyika Packers ulioko Kawe, Dar es Salaam. Mjini Kibaha mkoani Pwani kwenye Uwanja wa Tamco, Dodoma iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mtwara.
 

No comments:

Post a Comment